Tuesday, 23 February 2016

Kazimoto apandishwa kizimbani

KESI inayomkabili mchezaji mkongwe wa timu ya Simba Mwinyi Kazimoto ya shambulizi la kudhuru mwili dhidi ya mwandishi wa habari wa Kampuni ya Mwananchi Communications Ltd, Mwanahimba Richard imeanza kusikilizwa katika
Mahakama ya Hakimu Mfawidhi mkoa wa Shinyanga.
Akisomewa shitaka hilo mahakamani hapo na mwanasheria wa serikali, Upendo Shemkole alisema mshtakiwa alitenda kosa la shambulizi la kudhuru mwili Februari 10 mwaka huu, katika uwanja wa CCM Kambarage baada ya mazoezi. Ilielezwa mahakamani hapo kuwa mchezaji huyo alionekana kumshambulia mwandishi wa habari Mwanahimba Richard.
Hata hivyo, mshitakiwa Mwinyi Kazimoto baada ya kusomewa shitaka hilo alikana kutenda kosa hilo, na kuiomba Mahakama kumpatia mwezi mmoja ili atafute wakili wa utetezi wake, ombi ambalo lilikubaliwa.
Hakimu Mkazi Mfawidi wa mahakama hiyo, Rahim Mushi anayesikiliza kesi hiyo alisema imeahirishwa hadi Machi 21 mwaka huu, ndipo itaendelea tena kusikilizwa ili kutoa fursa kwa mshtakiwa kupeleka wakili wake wa utetezi.
Jumla ya mashahidi sita wanatarajiwa kutoa ushahidi mahakamani hapo katika kesi hiyo inayomkabili kiungo mchezaji wa Simba Mwinyi Kazimoto, ambapo pia alipatiwa dhamana Sh 500,000 na Mwanasheria wa Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, Batromeo Lwela.

0 comments:

Post a Comment