Hatimaye ile ripoti iliyokuwa inasubiriwa kwa hamu inayotishia hatima ya
ajira za watoto kadhaa wa vigogo ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT),
imekamilika na kuwasilishwa mezani kwa Rais John Magufuli, Ikulu.
Inasemekana kwa sasa hali si shwari BoT, baada ya kuwepo tetesi za
kupunguza watumishi ambao wengi ni watoto wa vigogo waliongia kwa
migongo ya wazazi wao.
==========================
Akizungumza na Nipashe jana, Gavana wa BoT, Prof. Benno Ndulu, alisema
maagizo ya Rais Magufuli juu ya kupitia upya ajira za watumishi wote wa
taasisi hiyo yameshafanyiwa kazi na ripoti yake imekamilika.
Machi 10 mwaka huu, Rais Magufuli alifanya ziara ya kushtukiza Makao
Makuu ya BoT na kutoa maelekezo mbalimbali kwa menejimenti ya taasisi
hiyo nyeti kwa mustakabali wa taifa kiuchumi.
Rais Magufuli alimuagiza Gavana wa BoT (Prof. Ndulu) kupitia upya ajira
za watumishi wa taasisi hiyo na kupunguza idadi ya watumishi hao hasa
ikibainika kuwa kazi zao zinaweza kufanywa na watu wengine.
Katika mazungumzo yake hayo na uongozi wa BoT, ilibainika kuwa benki
hiyo ina watumishi takriban 1,391; idadi ambayo ilionekana kuwa ni ya
juu kulinganisha na ukubwa wa taasisi hiyo na hivyo kumshangaza Rais
Magufuli.
Wakati akizungumza na Nipashe jana, Prof. Ndulu alisema kazi hiyo (ya
kupitia ajira za watumishi) ilishafanyika na ripoti yake
imeshawasilishwa kwenye vyombo husika.
"Hiyo kazi ilishafanyika kama alivyoagiza Mheshimiwa Rais na tayari
vyombo vinavyohusika vimeshapewa taarifa hiyo," alisema Prof. Ndulu na
kuongeza:
"Hatutoi taarifa kama hizo magazetini bali kwenye vyombo husika--sisi
tukishakamilisha kazi tunapeleka ripoti kwenye mamlaka husika na ndivyo
tulivyofanya."
AJIRA ZA WATOTO WA VIGOGO
Alipotembelea benki hiyo Machi, Rais Magufuli alisema anashangazwa
kuwapo kwa wafanyakazi wengi ndani ya BoT ambao baadhi hata kazi
wanazofanya hazijulikani wazi.
"Haiwezekani tukawa na kundi kubwa la wafanyakazi, wanalipwa mishahara
wakati hata kazi wanazofanya hazijulikani," alinukuliwa Rais Magufuli.
Kabla ya ziara ya Rais Magufuli, majina kadhaa ya watumishi wa BoT
yalikuwa yakiibua mijadala mbalimbali kwenye mitandao ya kijamii kwa
madai kuwa ajira zao zimetokana na kubebwa na wazazi ama ndugu zao ambao
wana ushawishi mkubwa serikalini kutokana na nafasi mbalimbali walizo
nazo au kuwahi kuwa nazo.
Orodha ya watu wanaodaiwa kuwa ni ya watoto wa vigogo, na ambayo Prof.
Ndulu alisema siyo mpya kwani ilishaandikwa na kujadiliwa sana hapo
kabla ni pamoja na Pamela Lowasa, anayedaiwa kuwa ni mtoto wa aliyekuwa
Waziri Mkuu, Edward Lowasa.
Wegine ni Filbert Sumaye anayedaiwa kuwa ni mtoto wa Waziri Mkuu mstaafu
katika serikali ya awamu ya tatu, Fredrick Sumaye na Zaria Kawawa,
anayedaiwa ni mtoto wa aliyewahi kuwa Waziri Mkuu katika serikali ya
awamu ya kwanza, Marehemu Rashid Mfaume Kawawa.
Mwingine ni Harriet Lumbanga anayedaiwa ni mtoto wa aliyewahi kuwa
Katibu Mkuu Kiongozi wakati wa utawala wa serikali ya awamu ya tatu,
Marten Lumbanga.
Aidha, orodha hiyo pia ina jina la Salama Ali Hassan Mwinyi anayedaiwa
ni mtoto wa aliyekuwa Rais wa awamu ya pili, Alhaji Hassan Mwinyi;
Rachel Muganda anayedaiwa ni mtoto wa aliyekuwa Balozi katika serikali
ya awamu ya nne, Alexender Muganda. Salma Omar Mahita, katika orodha
hiyo anadaiwa kuwa ni mtoto wa aliyekuwa Mkuu wa Jeshi la Polisi wakati
wa utawala wa awamu ya tatu, IGP mstaafu Omar Mahita.
Wengine ni Justina Joseph Mungai anayedaiwa kuwa ni mtoto wa aliyewahi
kuwa Waziri wa Elimu na Utamaduni katika serikali ya awamu ya tatu,
Joseph Mungai. Pia yumo Keneth Nchimbi anayehusishwa na kada wa CCM
aliyewahi kuwa kigogo wa Jeshi la Polisi John Nchimbi. Blasia William
Mkapa, anadaiwa kuwa ni mtoto wa Rais wa awamu ya tatu, Benjamin Mkpa
katika orodha hiyo yenye pia jina la Violet Phillemon Luhanjo, ambaye
anadaiwa kuwa mtoto wa aliyewahi kuwa Katibu Mkuu kiongozi wakati wa
serikali ya awamu ya tatu na nne, Phillemon Luhanjo.
Liku Kamba anadaiwa kuwa mtoto wa aliyekuwa kada wa CCM wa muda mrefu, Kate Kamba.
Wengine wanaotajwa katika orodha hiyo ni Thomas Mongela anayedaiwa kuwa
mtoto wa kada mashuhuri ndani ya CCM; aliyewahi kushika nyadhifa
mbalimbali zikiwamo za ubunge, Getrude Mongela. Jina la Jabir Abdalah
Kigoda linadaiwa kuwa ni mtoto wa aliyekuwa Waziri wa Viwanda na
Biashara katika serikali ya awamu ya nne, marehemu Abdalah Kigoda.
Machi mwaka huu, mara baada ya agizo la Rais Magufuli kuhusiana na ajira
za watumishi wa taasisi hiyo, Nipashe ilizungumza na Prof.
Ndulu kwa njia ya simu kutaka kujua kama kweli orodha ya watoto hao ni
miongoni mwa watumishi wa BOT na majibu yake kwa mwandishi, ambaye
alimsomea majina hayo kuanzia mwanzo hadi mwisho, ni kwamba orodha hiyo
'haina jipya'. Prof.
Ndulu alieleza zaidi kuwa hakuna ubaya wowote kwa mtu mwenye sifa kuajiriwa na BoT, bila kujali jina lake.
"Hayo majina kwani kwako wewe ni mapya? Mbona yameshaandikwa na
kujadiliwa sana hayo--mimi nasema hakuna jipya hapo," alisema Profesa
Ndulu na kuongeza:
"Hivi ukiwa na jina kubwa halafu ukiwa na akili ama sifa za kufanya kazi
fulani, unataka kuniambia usipewe hiyo kazi kwa sababu una jina kubwa?"
HOFU YATANDA
Licha ya ufafanuzi wa Prof. Ndulu kuhusiana na madai ya kuwapo kwa
watumishi walioajiriwa kwa sababu ya ushawishi wa wazazi wao ambao ni
vigogo serikali, bado mijadala mbalimbali iliendelea kutawala katika
mitandao ya kijamii kuhusiana na orodha hiyo.
Aidha, imedaiwa kuwa hofu imetanda miongoni mwa watumishi hao na wengine
wengi kutokana na kile kinachoelezwa kuwa huenda kukawa na punguzo
kubwa la watumishi kutoka idadi iliyopo sasa ya wafanyakazi 1,391; jambo
ambalo linaweza kutekelezwa wakati wowote kulingana na kile kilichomo
ndani ya ripoti na kumfikia Rais Magufuli.
Wengi wa wachangiaji katika mitandao ya kijamii kuhusiana na majina ya
watoto wa vigogo ni madai kwamba ajira zao zilitokana na ushawishi wa
majina makubwa ya wazazi wao katika medani za uongozi nchini na siyo
sifa za kuajiriwa kwenye taasisi hiyo na hivyo, upo uwezekano kuwa wengi
miongoni mwao hawatasalimika pindi kazi ya kuwapunguza watumishi (wa
BoT).
Source: Nipashe

0 comments:
Post a Comment